Habari

Imewekwa:: Oct, 19 2022
News Images

WAKULIMA WA PAMBA WAJIANDAA NA MSIMU MPYA WA KILIMO 2022-2023

Msimu wa Kilimo cha pamba kwa Kanda ya Magharibi inayoongoza kiuzalishaji nchini kwa asilimia 98 uanza tarehe 15 Novemba kila mwaka kwa kuzingatia kalenda ya msimu wa mvua katika maeneo mengi ya Kanda hii inayojumuisha mikoa ya Shinyanga, Simiyu, Mara, Tabora, Geita, Mwanza, Kagera, Singida, Katavi, Kigoma, Dodoma na Manyara

Ili kuweza kuendana vema na kalenda ya kilimo wakulima wa Pamba wametakiwa kuandaa mashamba mapema kabla ya msimu wa kupanda Haujafika kwa kufanya matayarisho ya kun'goa na kuchoma moto masalia ili kudhibiti mzunguko wa wadudu waharibifu wa zao Hilo pamoja na vimelea vya magonjwa.

Hayo yamebainishwa na Afisa kilimo Mwandamizi na Mkaguzi wa Pamba wilaya ya Igunga Mkoani Tabora Venance Kankutebe na kusema kuwa wakulima wanapaswa kuandaa mashamba mwezi mmoja kabla ya kuanza msimu wa kilimo.

Venance amesema kuwa wakulima wanapoandaa mashamba wanatakiwa kung'oa masalia kwa kuchimbua chini na kuondoa visiki kwani kwa kufanya hivyo atakuwa amepunguza ongezeko la wadudu ambao wangeweza kuzaliana kwenye masalia na kusababisha mashambulizi katika msimu unaofata.

"Visiki vikiachwa vitaota na kusababisha wadudu kuendelea kufanya mashambulizi na ndio maana tunawaimiza wakulima wanavyong'oa masalia waweze kutumia jembe kuondoa mche mzima pamoja na kuchoma moto" Alisema Venas.

Amefafanua kuwa wakulima wanapaswa kuzingatia kanuni za kuandaa Shamba mapema na kwa ufasaha kwa kufanya hivyo kutawasaidia kupanda Pamba Mara tu baada ya mvua zitakapoanza kunyesha na sio kusuburi mvua ianze kunyesha ndipo wanaanza kuandaa mashamba Kwa kufanya hivyo watasababisha Pamba kutokuota Kwa wakati.

" Ili upande Pamba Kwa wakati na uvune wakati sahihi ni lazima kuandaa Shamba lako mapema, lakini sasa wapo wakulima wanamsubiri mvua inyeshe ndio waandae Shamba ndio maana unakuta mtu anapata Pamba kinyume na matarajio aliyokuwa amejiwekea hiyo hayo yote yanatokana na ulimaji wa bila kufuata maelekezo kutoka kwa watalamu wa kilimo" Alisema Venance.

Saizi Ngusa na Amos Makalanga Ni wakulima wa zao la Pamba wameeleza kuwa Kuna umuhimu wa kuondoka masalia mashambani Mara baada ya kuvuna kwani Kwa kufanya hivyo kunawasaidia kuondoa wadudu waharibifu wa zao Hilo.

" Kwanza tukisha vuna Pamba alafu tukaondoa masalia shambani inatusaidia sana hususani katika msimu mwingine wa kilimo unapofika hatusumbuki sana kwa sababu Shamba linakuwa Safi" walisema.

Wameeleza kuwa elimu waliyoipata Kwa sasa imewasaidia na kilimo kimebadilika tofauti na zamani mtu alikuwa akilima anaacha masalia ya miti ya Pamba kukua na kuanza kuchipua tena, na kusubilia parizi hali iliyopelekea kutopata Pamba yenye ubora.

" lakini kwa sasa tunapokata masalia ya Pamba na kuyateketeza Kwa moto ili kuweza kuwaangamiza wadudu waharibifu ili msimu ujao wasiweze kuaribu Pamba kumetusaidia sana na kuona kilimo Cha Pamba ni kizuri zaidi kuliko kilimo kingine" Walisema.